HESLB na Hazina sasa komesheni udhaifu
Umekuwa ni kama
ugonjwa wa kudumu mwaka baada ya mwaka, wanafunzi wa elimu ya juu ni lazima
wagome kutokana na ama kukwama kwa mikopo kutoka Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa
Elimu ya Juu (HESLB) au kulalamikia utaratibu wa kutathminiwa ambao uamua
mwanafunzi akopeshwe kwa kiwango gani kuanzia asilimia 20 hadi 100.
Tunaweza kusema
kuwa kwa sasa kuna utamduni wa migomo katika vyuo vya elimu ya juu katika kudai
mikopo yao. Hata wanafunzi wenyewe wa elimu ya juu wanalijua hilo ndiyo maana
wengi wamesikika wakisema kuwa wanagoma ili fedha zao zitolewe.
Ni ada kugoma ili
fedha za mikopo zitolewe. Na kweli kila wanafunzi hawa wanapogoma basi hazipiti
siku mbili watu watakimbizana huko na huko na hatimaye fedha zitafikishwa ama
kwenye akaunti zao moja kwa moja au hata vyuoni kwao.
Itakumbukwa
kwamba mwaka juzi mwishoni vyuo vya elimu ya juu vilichelewa kufunguliwa kwa
sababu ya madai kwamba mchakato wa kuweka mambo sawa ulikuwa ukiendelea ikiwa ni
pamoja kuepuka migogoro ya kila wakati kwamba wanafunzi wanafika vyuoni lakini
kunakuwa hakuna fedha kutoka Bodi ya Mikopo.
Kuchelewa
kufunguliwa kwa vyuo hivyo mwaka juzi kulizua malumbano ya kisiasa yakijielekeza
kwenye hisia kwamba wanafunzi wapatao 60,000 hivi wa vyuo hivyo wangekosa haki
yao ya kupiga kura; huku wengi wakienda mbali zaidi na kudai kwamba zilikuwa ni
njama za kupunguza kura za baadhi ya wagombea.
Vyombo mbalimbali
vya kiserikali vilivyotoa kauli kuhusu hilo vilisisitiza juu ya kuchelewa
kufunguliwa huko kuwa kulitokana na ulazima wa kukamilisha taratibu muhimu za
kudahili wanafunzi, lakini pia kuhakikisha kwamba kila kitu kinafanikiwa kabla
ya vyuo hivyo kufunguliwa.
Ni jambo la ajabu
kuona kwamba kumbe hata baada ya kuchelewa kufungua vyuo kwa kiasi hicho, bado
mikopo ya wanafunzi haijashughulikiwa ipasavyo kiasi cha kuwa chanzo cha
migomo.
Wanafunzi wa
Mkwawa kipindi fulani waliozungumza na kusema kuwa walikuwa wamekaa
kwa siku tatu bila chakula kwa sababu mikopo yao kutoka Bodi ya Mikopo ilikuwa
haijatolewa.
Tunasikitika
kwamba hali hii inawapata wanafunzi ambao wanalazimika kukatiza masomo na
kuingia katika mapambano na dola ili kupata haki yao. Ni jambo baya na ambalo
hakika halistahili kuungwa mkono kwamba uzembe unaruhusiwa kuota mizizi katika
utekelezaji wa majukumu wa watumishi wa umma kiasi cha kuwafanya wajenge
utamaduni wa kudai haki kwa migomo mwaka baada ya mwaka.
Tunaamini kwamba
HESLB wanajua fika kwamba vyuo vinafunguliwa lini, wanajua wanafunzi walio na
sifa za kupewa mikopo ni wangapi ni nani, lakini pia wanajua fika kwamba ulipaji
wa fedha kutoka benki moja hadi nyingine hapa nchini huchukua muda gani, ili kwa
kuzingatia hayo yote wahakikishe kwamba malipo ya wanafunzi yanawafikia kwa
wakati.
Kama kikwazo ni
Hazina, kwa maana ya kutoa fedha kwenda HESLB nako hali ni hiyo hiyo, wanajua
wanafunzi wanahitaji kula, wana gharama nyingine tu za kulipa na kipato pekee na
cha hakika kwa wale walio na sifa ya kukopeshwa ni mkopo husika ambao hulipwa
kwa utaratibu mahususi uliokubalika, aghalab kila mwezi.
Kwa maana hiyo,
hakuna asiyejua umuhimu wa kuwajengea wanafunzi hawa mazingira mazuri ya kusoma
ikiwa ni pamoja na kuwahakikisha kwamba wanalipwa fedha zao kwa wakati ili isiwe
sababu ya kuvuruga taratibu nyingine za masomo.
Kila tunapoona
hali ya migomo katika vyuo vya elimu ya juu ikijirudia mwaka baada ya mwaka
sababu zikiwa ni zile zile, yaani kucheleweshwa kwa mikopo ya wanafunzi kutoka
HESLB tunaanza kujawa na hofu kwamba huenda wapo wanaonufaika na hali hii,
vinginevyo kwa nini haikomeshwi?
Tunafikiri wakati
umefika sasa HESLB au Hazina kujisafisha na lawama hizi kwa kuwawajibisha wote
wanaosababisha usumbufu huu ambao kimsingi unalea nautamaduni wa migomo vyuoni. Sisi tunasema hali hii haikubaliki. kukuza
No comments:
Post a Comment